Kufafanua lebo ya faragha ya WhatsApp katika Duka la Programu la Apple
Hivi majuzi Apple walihitaji kuwa programu zote zinazosambazwa kupitia Duka la Programu zionyeshe maelezo yanayolenga kuwaonyesha watu jinsi data yao inaweza kutumiwa. Tunaunga mkono juhudi za kuleta uwazi, ndiyo maana tayari tunatoa njia kwa watu kupakua taarifa zinazohusiana na akaunti zao. Huwa tunafanya juhudi kubwa kutengeneza WhatsApp kwa njia inayolinda faragha ya watumiaji wetu na huwa tunawafahamisha hili mwanzoni mwa kila mazungumzo.
Tulitekeleza ufumbaji wa mwisho hadi mwisho kote kwenye programu yetu katika mwaka wa 2016, kumaanisha kuwa simu, ujumbe, picha, video na ujumbe wa sauti kwenda kwa marafiki na familia hushirikiwa na wapokeaji wanaolengwa tu; na si mtu mwingine yeyote (si hata sisi) anayeweza kuyasoma. Kwa kutumia ufumbaji wa mwisho hadi mwisho, ujumbe hauhifadhiwi kwenye seva zetu baada ya kuwasilishwa, na katika hali ya kawaida ya utekelezaji wa huduma zetu huwa hatuweki rekodi ya watu unaoweza kuwatumia ujumbe.
Ni lazima tukusanye taarifa fulani ili kutoa huduma thabiti ya kimataifa. Kimsingi, huwa tunapunguza aina ya data tunayokusanya. Kwa aina ndogo ya data tunayokusanya, huwa tunachukua hatua ya kudhibiti ufikiaji wa taarifa hizo. Kwa mfano, ingawa unaweza kutupa idhini ya kufikia waasiliani wako ili kusaidia kufikisha ujumbe unaotuma, huwa hatushiriki orodha za waasiliani na mtu yeyote, ikiwa ni pamoja na Facebook kwa matumizi yake. Tunatoa maelezo zaidi kote kwenye Kituo chetu cha Msaada, Sera ya Faragha, na Masharti ya Huduma.
Hapa chini tunatoa ufafanuzi kuhusu lebo ya WhatsApp inayoonyeshwa kwenye Duka la Programu ya Apple na maelezo ya ziada kuhusu matumizi ya data ambayo hailindwi na ufumbaji wa mwisho hadi mwisho. Ni muhimu kuelewa kuwa maelezo kadhaa hapa chini yanatumika katika vipengele visivyo vya lazima ambavyo watu wanaweza kuchagua kutumia; hatukusanyi kiotomatiki kila maelezo hapa chini. Nyingi ya vipengele hivi visivyo vya lazima, kama vile ununuzi na malipo, vinatumika kwenye WhatsApp pekee na havitolewi na watoa huduma wengine wa utumaji ujumbe uliofumbwa mwisho hadi mwisho.
- Maelezo ya mwasiliani: Unapojisajili kwenye WhatsApp, tunapokea nambari yako ya simu na tunaitegemea ili kufikisha ujumbe kwenye kifaa chako. Ikiwa ungependa kuwasha uhakiki wa hatua mbili, unaweza kuchagua kushiriki anwani yako ya barua pepe na WhatsApp, ingawa si lazima. Vile vile, unaweza kuchagua kutuma barua pepe kwa WhatsApp ili upate msaada.
- Vitambulishi: Tunahusisha nambari yako ya simu na Kitambulisho chako cha mtumiaji cha WhatsApp na tunafahamu anwani ya IP unayotumia kuunganisha simu yako kwenye WhatsApp.
- Mahali palipokadiriwa: Ingawa huwa hatuoni kamwe mahali halisi ulipo, tunafahamu anwani yako ya IP na msimbo wa nchi kutoka kwenye nambari yako ya simu.
- Waasiliani: Kukurahisishia kutuma ujumbe kwa marafiki na familia yako, unapojisajili kwenye WhatsApp huwa tunaomba idhini ya kufikia nambari zako za simu ili kuona nambari zilizothibitishwa kwenye mfumo wetu. Ukiamua kufanya hivyo, programu huonyesha majina unayochagua kutoka kwenye kitabu cha anwani na hatushiriki taarifa yoyote katika hizi na Facebook. Pata maelezo zaidi hapa.
- Data ya matumizi: Ili kutekeleza huduma inayoaminika kimataifa, ni sharti tuelewe iwapo vipengele vinafanya kazi ipasavyo, ingawa tunafanyia majaribio mbinu ya kufanya hivi katika njia isiyotambulika. Ili kuzuia matumizi mabaya tunachukua hatua dhidi ya akaunti zinazojishughulisha katika utumaji ujumbe kiotomatiki au ujumbe mwingi kwa wakati mmoja, hatua ambayo imekuwa muhimu hasa wakati wa uchaguzi ambapo makundi fulani yanaweza kujaribu kutuma ujumbe mwingi kwa wakati mmoja. Huwa tunafadhili pia kampeni za matangazo, ikiwa ni pamoja na kutumia mtandao wa matangazo wa Apple, kuwafikia watu ambao hawatumii WhatsApp kwa sasa. Huwa tunawasiliana pia na watumiaji ndani ya programu kuhusu vipengele vya bidhaa na masasisho mapya na kutoa elimu kwa watumiaji.
- Uchunguzi: Ukikabiliwa na tatizo wakati wa kutumia WhatsApp huwa tunapokea kumbukumbu ya matukio ya programu kuacha kufanya kazi ili tuweze kurekebisha hitilafu na kuboresha huduma yetu.
Machaguo ya ziada tunayotoa:
- Maelezo ya fedha: Katika nchi ambako unaweza kutuma malipo kupitia WhatsApp, maelezo yako ya kadi au benki yanahitajika ili kukamilisha muamala.
- Ununuzi: Ukichagua kutumia Maduka ya Facebook kwenye WhatsApp, tunaweza kuelewa shughuli yako ya ununuzi, kama vile bidhaa unazoangalia na kununua na tunaweza kushiriki maelezo haya na Facebook kwa kuwa Maduka ni bidhaa ya Facebook. Hii ina maana kuwa hali yako ya utumiaji wa kuvinjari kwenye bidhaa na kununua kwenye Maduka kunaweza kushawishi unachoona kwenye Maduka na kwenye bidhaa zingine za Facebook. Kabla ya kutumia Maduka ya Facebook kwenye WhatsApp, tunakueleza kuhusu hili na tunakuomba idhini.
- Maudhui ya mtumiaji: Huwa tunapokea taarifa zako za “kuhusu” pamoja na picha ya jalada, majina ya vikundi, picha ya jalada ya kikundi na maelezo ya kikundi. Tunategemea taarifa hii kuzuia matumizi mabaya, ikiwa ni pamoja na kupiga marufuku akaunti zinazoshiriki picha za unyanyasaji wa watoto. Vile vile, ukiamua kuripoti tatizo kwa WhatsApp, tutapokea utakachoamua kututumia.